MKE wa Rais, Mama Salma Kikwete, ametimiza ahadi yake kwa Miss World Africa, Nancy Sumary, ya kumkaribisha Ikulu, Dar es Salaam, na kumpongeza kwa kutwaa taji hilo.
Utekelezaji wa ahadi hiyo ulifanyika juzi usiku, ambapo Mama Salma alimwandalia mrembo huyo tafrija maalum.
Mama Salma aliahidi kumkaribisha Nancy, Ikulu na kumwandalia tafrija, alipompokea mwaka jana uwanja wa ndege wa Mwalimu Nyerere, Dar es Salaam, mlimbwende huyo aliporejea kutoka Sanya, China ambako alishiriki mashindano ya kumsaka mrembo wa dunia na kufanikiwa kutwaa taji la Miss World Africa.
Katika hafla ya juzi, Mama Salma alikamilisha azma yake hiyo kwa kumzawadia Nancy seti ya mkufu, ambayo thamani yake haikuweza kufahamika.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mama Salma aliwashauri wazazi kuwaendeleza watoto wao katika sanaa kwa kuwaruhusu mabinti zao kushiriki katika masuala mbalimbali ya kisanii, yakiwemo mashindano ya urembo.
Pia wasanii kadhaa wakiwemo, Miss World Tourism (Africa), Witness Manwingi, walihudhuria, sambamba na viongozi mbalimbali akiwemo Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba.
Alisema kipindi kilichopo si cha kusema kuwa mwanamke ni mtu wa kufanya shughuli za jikoni pekee, bali kauli hizo na nyingine ambazo zinamkandamiza mwanamke zimepitwa na wakati.
“Wanawake tusikubali kuishia hapa tulipo. Kama wewe ni msanii jitume kufanya mambo makubwa zaidi kupitia usaniii wako. Kadhalika jifunze mbinu na taratibu za kufika unakotaka kufika. Na kama ni elimu basi hakikisha una elimu ya kutosha, “ alisema.
Nancy alimshukuru Mama Salma kwa kutekeleza ahadi yake ya kumkaribisha Ikulu, hali aliyoielezea kuwa inathibitisha jinsi anavyojali mafanikio ya wanawake.